.

.
.

.

.
.

.

.
.

.

.
.

.

.
.

.

.
.

.

.
.

Wednesday, February 26, 2014

Taswira Bunge Maalum la Katiba: Rasimu ya Kanuni za Bunge Maalun yawasilishwa



Kamati ya Kumshauri Mwenyekiti wa Muda wa Bunge Maalum Kuhusu Kanuni za Bunge Maalum imemaliza kazi yake na kuwasilisha Rasimu ya Kanuni za Bunge Maalum 2014.

Akiwasilisha Taarifa ya Kamati hiyo kwenye semina ya Wajumbe wa Bunge Maalum,  Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Profesa Costa Ricky Mahalu amesema kazi ya Kamati yake ilifanyika kwa muda wa siku sita kwa kupitia na kuchambua kwa kina rasimu ya Kanuni za Bunge iliyokuwa imeandaliwa na Kamati ya Maandalizi ya Bunge Maalum chini ya usimamizi  Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Katibu wa Baraza la Wawakilishi, Zanzibar.

Kamati hiyo imepitia Sehemu zote kumi na moja za rasimu ya awali na kushauri marekebisho na mapendekezo mbalimbali ambayo yatapitiwa na wajumbe wote wa Bunge Maalum kabla ya  kupitisha Azimio la kuridhia Kanuni za Bunge Maalum.  Kupitishwa kwa Azimio la Kanuni hizi kutawezesha uchaguzi wa Mwenyekiti wa kudumu wa Bunge Maalum pamoja na utaratibu wa Kiapo kwa Katibu na Naibu Katibu wa Bunge Maalum, kiapo kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Bunge Maalum , kiapo kwa Wajumbe wa Bunge Maalum na hatimaye uwasilishwaji na mjadala wa rasimu ya Katiba. Aidha, Kamati imependekeza kuwa kura zote zitakazopigwa ziwe za siri.

Aidha, Kamati imepekeza kuwa Siwa itakayotumika katika Bunge Maalum ihifadhiwe baada ya kupatikana kwa Katiba mpya ili iwe ukumbusho wa kihistoria.  Siwa hiyo iwe na kichwa cha dhahabu, kitabu (kuashiria Katiba), alama ya watu wa makundi mbalimbali, rangi za taifa, nembo ya taifa na alama ya kalamu kama kielelezo cha uandishi.
 
Baada ya taarifa kuwasilishwa Semina iliahirishwa ili kutoa fursa kwa wajumbe kuipitia rasimu mpya ya Kanuni na kujiandaa kwa mjadala.

Taarifa na matukio zaidi tembelea Kituo cha Habari , Maktaba ya Picha katika tovuti hii.